Uchaguzi mkuu DRC: EU yalaani balozi wake kufurushwa DRC

Congolese National Police arrest a man in Goma, on December 27, 2018

Chanzo cha picha, Getty Images

Maelezo ya picha,

Polisi walipambana na wafuasi wa upanzi mashariki mwa DRC Alhamisi

Muungano wa Ulaya umeukosoa uamuzi wa Jamhuri ya Demokrasi ya Congo kwa kumfukuza balozi wake kabla ya uchaguzi muhimu nchini humo siku ya Jumapili.

"Amri ya kumtaka Bart Ouvry kuondoka ndani ya saa 48 ni kinyume kabisa na sheria", msemaji wa EU alisema.

DR Congo ilisema ilichukua uamuzi huo kulipiza vikwazo alivyowekewa mgombea wa chama tawala Emmanuel Ramazani Shadary.

Maandalizi ya uchaguzi huo yamekumbwa na ghasia.

Supporters of Congolese joint opposition Presidential candidate Martin Fayulu, gesture as they protest over their exclusion from the presidential election in Beni, Democratic Republic of Congo

Chanzo cha picha, Reuters

Maelezo ya picha,

Wafuasi wa Martin Fayulu wakiandamana mjini Beni

Siku ya Alhamisi wafuasi wa upinzani walivamia kituo cha Ebola kwenye mji ulio mashariki wa nchi wa Beni kupinga uamuzi wa tume ya uchaguzi wa kuahairisha uchaguzi kwenye miji mingine miwili hadi mwezi Machi.

Ghasia pia zilizuka kwenye miji miwili ngome za upinzani ya Goma na Butembo iliyo yote mashariki mwa nchi.

Tume ya uchaguzi ilisema uchaguzi kwenye miji wa Beni, Butembo na mji ulio magharibi wa Yumbi utaahirishwa hadi Machi kwa sababu ya ukosefu wa usalama na mlipuko wa ugonjwa wa Ebola eneo la mashariki umesababisha vifo vya zaidi ya wtu 300.

DRC voting official tests a voting machine

Chanzo cha picha, Reuters

Maelezo ya picha,

Maafisa wa uchaguzi wamekuwa wakifanyia majaribio mashine kabla ya uchaguzi

Kipi kilisababisha kuzuka mzozo wa kidiplomasia?

Vikwazo kwanza vilitangazwa dhidi ya Bw Shardary mwaka 2017 kwa ukiukaji wa haki za binadamu ikiwemo hatua kali dhidi ya upinzani.

Tarehe 10 Desemba mawaziri wa EU waliongeza vikwazo hivyo vikiwemo vya kuzuia mali na marufuku ya kusafiri kwa Bw Shardary na watu wengine 13 kwa kuhujumu uchaguzi na ukiukaji mwingine wa haki za binadamu.

Siku ya Alhamisi waziri wa mashauri ya nchi za kigeni nchini DRC Leonard She Okitundu, alisema serikali ilikuwa imeitaka EU kufuta vikwazo hivyo hadi baada ya uchaguzi lakini ilikataa.