"Mwanangu aliniomba nimpake rangi nyeupe kuepuka ubaguzi''

Chanzo cha picha, Getty Images
"Baba, kwa nini tusichukue hiyo rangi iliyobaki nyumbani na kunipaka mimi, wewe na kaka yangu? Sote tukijipaka rangi nyeupe hatutapata shida tena."
Kauli hiyo ilitolewa na mtoto wake wa kiume wakiwa bafuni huku wakichezea na povu hilo na anasema ni mara ya kwanza hali hiyo ilimuathiri sana.
"Kusema kweli, machozi yalinitoka," anasema baba mmoja anayeishi na familia yake kusini mwa Uingereza.
Kufikia wakati huo walikuwa wameteseka kutokana na unyanyasaji wa kibaguzi kutoka kwa majirani kwa miaka mingi.
Unyanyasaji huo ulikuwa mkubwa kiasi kwamba walilazimika kubadili nyumba, kazi, shule, kwa kuogopa, wanasema, kwamba nyumba yao ingechomwa.
Hakuna faini wala amri ya zuio iliyoweza kumzuia.
Walihamishwa msimu uliopita wa kiangazi kwa usaidizi wa shirika lisilo la faida la Sovereign Housing, ambalo halijatoa maoni kuhusu suala hilo.
Chanzo cha picha, Getty Images
Unyanyasaji huo ulianza Septemba 2017.
"Haikutarajiwa kabisa," baba huyo anasema.
"Tuliendesha gari na watoto wakaanza kurudi nyumbani. Nilisikia mtu akipiga kelele, 'Weirdo!' "Anakumbuka.
"Nilitazama na kumuona huyu jamaa, jirani yetu mmoja, amesimama upande wa pili akirusha matusi," anaendelea.
"Walianza kukaribia zaidi na zaidi. Walikusanyika na kupiga kelele zaidi za kibaguzi."
Chanzo cha picha, Getty Images
Familia iliripoti dhuluma hiyo kwa polisi na majirani waliitwa kufika mahakamani.
Mmoja wao, mwanamke, alikiri kutenda kosa la ubaguzi wa rangi na alitozwa faini ya pauni 200 (kama dola za Kimarekani 265) mnamo Novemba 2017.
Na faini hiyo hiyo ilipokea mwingine wa majirani, mwanaume, mnamo Januari 2018.
Shirika la Sovereign Housing, ambacho kinamiliki nyumba kote kusini na magharibi mwa Uingereza, kilikuwa kimewasilisha kesi ya madai dhidi yao baada ya wafanyakazi wao "kushtushwa na vitisho vya vurugu" vilivyopokelewa na familia.
Pamoja na hayo, familia inasema unyanyasaji huo uliendelea na hakuna hatua zaidi zilizochukuliwa.
"Tutakutafuta, tutakuchoma nyumbani kwako,' walitufokea," baba huyo anasema.
"Nilikuwa na ndoo tayari kujaza maji ikibidi, kwa sababu nilikuwa na wasiwasi kuwa watu hawa wangechoma moto nyumba tukiwa ndani."
Chanzo cha picha, Getty Images
Kitengo cha polisi kinachoshughulikia malalamishi ya unyanyasaji kwa misingi ya rangi kilisema maafisa walikuwa wamezungumza na mashahidi wa kujitegemea ndani ya saa 48 baada ya malalamiko ya kwanza.
"Tunajua kwamba uhalifu wa chuki una athari kubwa kwa waathiriwa, familia zao na jamii kwa ujumla," msemaji wa polisi alisema.
"Tunataka wakazi wetu wajue kwamba tunachukulia ripoti zote za uhalifu wa chuki kwa uzito mkubwa na kwamba msaada unapatikana kwa ajili yao."
Huduma ya Waendesha Mashtaka wa The Crown (CPS) inasema imeomba mahakama kutoa hukumu za juu zaidi kwa wanyanyasaji, ambao walipokea faini kubwa zaidi, zinazolingana na tabia ya kibaguzi.
"Tunatambua kwamba waathiriwa katika kesi hii wameteseka sana kutokana na dhuluma za kibaguzi kutoka kwa majirani zao," alisema msemaji wa CPS.
"Hakuna mtu anayepaswa kuishi kwa hofu ya kuwa mwathirika, na imedhihirika kuwa wamevumilia lugha ya kuudhi sana."
"Washtakiwa walifunguliwa mashtaka kwa kutumia lugha ya kuudhi ya rangi."
BBC iliwasiliana na Sovereign Housing, lakini haijatoa maoni yoyote kuhusu kesi hiyo.