Endrick: Kinda huyo wa Brazil anafananishwa na Neymar na tayari amevutia klabu kuu kutoka Ulaya

Chanzo cha picha, @Endrick11 on Twitter
Endrick, 15, alishinda tuzo ya mchezaji bora wa mashindano wakati timu yake ya Palmeiras iliponyanyua Kombe la Copa Sao Paulo, mashindano ya kwanza ya Brazil y wachezaji walio chini ya umri 21, mnamo Januari.
Palmeiras na Oeste walipomaliza mpambano wao Januari 19, maskauti kutoka Barcelona, Arsenal, Liverpool, Manchester City, Southampton, Ajax na Benfica wote walikaa viti vyao tayari kwa robo-fainali ya Copa Sao Paulo, shindano kuu la vijana la Brazil.
Wengi wao walikuwepo kumtazama Endrick. Mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 15 alitwaa taji la vijana chini ya umri wa miaka 21, akiwa amefunga mabao manne hadi kufikia hatua hiyo na kutoa mchango mkubwa zaidi kuliko nyota wa Brazil na Paris St-Germain Neymar akiwa na umri huo.
Wengi hawakuweza kutarajia, kile ambacho walikuwa karibu kuona.
Dakika ya 13 mpira ulidondoka nyuma ya chipukizi huyo wa Palmeiras na, bila kufikiria sana, akaupiga teke la baiskeli kutoka nje ya eneo la goli na kuutia wavuni mpira huo
"Nadhani tunaweza kuwa tunaona vipaji maalum sana vinavyojitokeza," alisema mtangazaji wa Mechi ya siku au Match of the Day, Gary Lineker.
Ghafla, alifananishwa na gwiji wa Brazil Ronaldo na baadhi ya washambuliaji mahiri wa nchi hiyo i.
Endrick hakuishia hapo, alifunga bao katika ushindi wa 4-0 dhidi ya Santos na alitajwa kuwa mchezaji bora wa michuano ya Copinha, kama mashindano hayo yanavyojulikana.
"Sikumbuki mchezaji mwingine yeyote wa umri wake katika historia ya hivi majuzi akifanya alichofanya," mshauri wake Frederico Pena, mtendaji mkuu wa TFM - wakala sawa wa michezo anayefanya kazi na Vinicius Jr wa Real Madrid na Gabriel Martinelli wa Arsenal - aliiambia BBC Sport.
"Jinsi alivyoshughulikia shinikizo zote ilivutia kwa sababu wakati mwingine unaona mtoto anacheza mchezo mzuri na anashindwa kudumisha kiwango sawa cha uchezaji. Hilo halikutokea kwake. Licha ya kuambukizwa Covid-19 wakati wa kampeni, kwa kweli. Ameimarika zaidi
Hatahivyo wale wanaomjua hwakushangaa kwani, mwaka jana, aliichezea Palmeiras katika fainali ya Mashindano ya Jimbo la Sao Paulo katika vikundi vya umri wa chini ya miaka 15, 17 na chini ya 20.
Wengi nyumbani walitaka ajumuishwe kwenye kikosi ambacho mabingwa hao wa Amerika Kusini wangeshiriki kwenye Kombe la Dunia la Vilabu huko Falme za Kiarabu mwezi huu. Lakini kocha wa Ureno Abel Ferreira alifutilia mbali uwezekano wowote wa Endrick kushiriki katika mechi hizo ambazo huenda wakapangwa dhidi ya Chelsea. Bila kujali hilo , inaonekana ni muda tu kabla ya kinda huyo kujiunga na klabu kubwa.
Kukabiliana na changamoto ndani na nje ya uwanja
Babake Endrick Douglas Sousa hatasahau siku ambayo mtoto wake alikuja kwake akiomba chakula huko kwao Brasilia - na hakuwa na cha kumpa.
Sousa alipokuwa akilia, alimsikia Endrick akiahidi kuwa atakuwa mchezaji was oka ili kuboresha hali yao.
Akiwa na kipaji cha asili, mshambuliaji huyo chipukizi alijipata kwenye rada ya Sao Paulo, lakini hawakuweza kufikia makubaliano kwani walikuwa tayari kutoa posho la kila mwezi la £25 pekee kusaidia familia hiyo.
Ni wakati, huo Endrick akiwa na umri wa miaka 11, ambapo wapinzani wao Palmeiras walijitokeza na kuhitimisha usajili wake.
"Nilikuwa nimepokea video yake akicheza huko Brasilia na nilipenda sana nilichokiona, kwa hivyo nilitoa OK kwa ofa ambayo ingewaruhusu kuwakodishia nyumba huko Sao Paulo," Joao Paulo Sampaio, mshiriki wa kandanda ya vijana wa Palmeiras alisema.
"Na Endrick alionesha mchezo mzuri kutoka dakika ya kwanza. Mara baada ya kuwasili, alifunga bao la teke la baiskeli katika sare ya mkondo wa kwanza dhidi ya Santos kwenye fainali ya Ubingwa wa Jimbo la U-11. Kisha, katika mkondo wa pili kukiwa na zaidi ya mashabiki 22,000 wa nyumbani wakitazama, alisaidia timu yake kushinda taji hilo . Yuko hivi. Kila mara tunapompatia changamoto anakabiliana nayo vyema."
Haikuwa rahisi kwa familia ya Sousa katika nyumba yao mpya.
Katika miezi yake sita ya kwanza huko Sao Paulo, babake Endrick alibaki bila kazi na aliuza chai katika kituo cha basi cha Barra Funda ili kupata pesa. Muda kidogo baadaye, aliandikwa kazi ya kusafisha na klabu ya Palmeiras. Wakati mwingine, aliweza kula na wachezaji wa kikosi cha kwanza, lakini angekunywa supu pekee. Hilo lilimvutia kipa Jailson, ambaye aligundua kuwa Sousa alikuwa na meno saba pekee na alilipia matibabu yake ya meno.
Changamoto hizo kwasasa zimekwisha, hata hivyo. Baada ya mafanikio ya hivi majuzi ya Endrick, babake aliwacha kazi ya kusafisha katika klabu hiyo.
Ni zaidi ya Romario na Ronaldo?
Chanzo cha picha, Placar
Endrick ndiye nyota wa jarida la Placar la mwezi huu, jarida maarufu la michezo nchini Brazili
Licha ya umri wake mdogo , chipukizi huyo wa Brazil amevutia wengi sio tu kwa ufungaji wake wa magoli bali pia ana pua inayoweza kunusa magoli lakini pia ni mchezaji anayejitolea
"Tuna mifano miwili ya Vinicius Jr na Martinelli na tunazungumza mengi kuwahusu, tukimuonyesha jinsi maisha yao ya kila siku yalivyo, jinsi walivyokabiliana na matatizo na pia kutunza miili yao," Pena alisema.
"Ilikuwa ngumu sana kwa wote wawili kufika walipo sasa. Vinicius alipitia nyakati ngumu akiwa Real Madrid, ambapo baada ya kufanya mambo mengi na kuonekana kama amefanikiwa, alijikuta nje ya vikosi vya siku ya mechi.
"Martinelli, pia, ameanza kurudi kucheza tena katika kikosi cha kwanza, lakini alikaa karibu mwaka mzima Arsenal bila kushiriki mechi . Kwa hivyo tunamweleza kuwa haijalishi kama wewe ni mchezaji wa kiwango cha juu, bado utalazimika kufanya kazi kwa bidii mara mbili.
"Ana mawazo haya na pia anafanya juhudi nje ya klabu. Miongoni mwa mambo mengine, tunalipa kipaumbele suala maalum la chakula chake, kwa mfano, alikuwa na Toddynho [maziwa ya chokoleti yaliyo tayari kunywa huko Brazil] wakati wa kifungua kinywa na tayari ameacha kunywa . Tayari ana asilimia kubwa ya kusajiliwa kaa mchezaji wa kulipwa."
Hakuna anayetilia shaka kwmba Endrick ndiye mchezaji mkubwa chipukizi Brazil - ameangaziwa kwenye ukurasa wa mbele wa gazeti la Uhispania la Marca mara tatu ndani ya wiki kadhaa huku kukiwa na uvumi unaomhusisha na kujiunga na Barca na Real Madrid.
Inapokuja kwake, inaonekana kuna wasiwasi mmoja tu kati ya maskauti wa kimataifa - kimo chake cha futi 5 inchi 6 (1.73m).
"Haonekani kuwa mchezaji ambaye atafikia urefu wa 5ft 9in (1.80m), ambayo inaweza kuwa mfano bora kwa fowadi ikiwa tutamkumbuka Ronaldo," aliongeza Pena.
"Atakuwa mwanariadha mfupi zaidi, pengine urefu wa 5ft 7 hadi 5ft 8in. Lakini ikizingatiwa kwamba mmoja wa washambuliaji bora wa wakati wote nchini alikuwa Romario na alikuwa na urefu wa futi 5 na inchi 4, ni salama kusema atakuwa sawa."
Kwa sasa, Endrick hawezi kucheza soka ya wakubwa au kusaini mkataba wake wa kwanza wa kulipwa nchini Brazil hadi atakapofikisha umri wa miaka 16 mwezi Julai.
Vilabu vingi vitakuwa vinangoja kwa hamu wakati huo, ingawa sheria za Fifa zinamaanisha kuwa hataweza kuhamia Uropa hadi atakapofikisha miaka 18.
Inawezekana kufikia makubaliano na timu nyingine kabla ya umri huo, hata hivyo, kitu ambacho Real Madrid walifanya na Vinicius Jr walipotangaza mwaka 2017 mkataba wa euro 45m (£37.7m) kumsajili fowadi huyo, ambaye alijiunga nao mwaka uliofuata.
Ripoti za Uhispania hata zinaonyesha Real Madrid wako tayari kuendana na ada waliyolipa Vinicius Jr kumleta Endrick Ulaya.
"Hakuna kitu kinachotokea kwa sasa," Pena alisema. "Tutawezaje kuuza mchezaji ambaye anaweza tu kuondoka mnamo 2024?
"Hatujawahi kuona mtu akijadiliwa miaka miwili kabla ya kuhama, lakini ni wazi kuwa kuna mara ya kwanza kwa kila kitu na anaweza kuwa wa kwanza."
Chanzo cha picha, BBC Sport